Sababu za Mwanamke Kukosa Hamu ya Tendo la Ndoa na Suluhisho lake - bongo specially

Breaking

Post Top Ad

Thursday 14 September 2017

Sababu za Mwanamke Kukosa Hamu ya Tendo la Ndoa na Suluhisho lake



Hili ni tatizo ambalo nimekuwa nikiulizwa mara nyingi sana na wanawake wengi kwa muda sasa na mwanzoni nilikuwa nalichukulia poa lakini kadri siku zinavyoenda naendelea kuona wengi zaidi wakizidi kunitafuta kwa ajili hii.

Wapo ambao wameshakuja hata kuniona kwa macho kwa ajili ya tatizo hili. Kweli unaweza ukadhani ni utani lakini ni tatizo linalozidi kuongezeka katika jamii yetu miaka ya sasa.

Na tatizo linakuwa baya zaidi kama linatokea ndani ya ndoa, kwani sababu hasa ya ndoa ni hiyo, kama ni kupika mwanaume anaweza kula hotelini au hata kujipikia mwenyewe kama ni kufua siku hizi kuna mashine za kufulia zinazotumia umeme nk nk

Na kama kuna jambo linaweza kuharibu ndoa yako taratibu bila wewe mwanamke kujua basi ni kumnyima haki ya ndoa mwenza wako kwa kisingizio cha eti huna hamu ya kushiriki tendo la ndoa!

Hili linapokutokea jaribu kufanya kila uwezalo ili uweze kurudi kwenye hali yako kama mwanzo.

Ni jambo la kawaida kabisa kumkuta mwanaume akinunua dawa ya kuongeza nguvu au hamu ya kushiriki tendo la ndoa lakini ni kinyume kwa wanawake.

Hata hivyo kuna ongezeko kubwa la kina mama wanaopungukiwa na hamu ya kutaka kushiriki tendo  la ndoa na wengine wanalichukulia ni jambo la kawaida jambo ambalo ni hatari kwa mahusiano yako na mwenza wako.

Kama una umri wa miaka 45 kushuka chini na unapatwa na tatizo hili, somo hili lina msaada mkubwa kwako katika kukabiliana na tatizo la kukosa hamu ya kutaka kushiriki tendo la ndoa.



Sababu za mwanamke kukosa hamu ya kushiriki tendo la ndoa

1. Ugomvi kwenye mahusiano
Kugombana kila mara na mwenza wako ndiyo namna rahisi kabisa inayoweza kuua hamu yako ya kutaka kushiriki tendo la ndoa.

Unapokuwa na hasira au umechukizwa na mwenza wako basi tendo la ndoa ndilo jambo la mwisho kabisa linaweza kukujia kichwani mwako.

Kuepuka hili jitahidi kupunguza ugomvi kwenye mahusiano yako na kama tayari yapo basi muwaone washauri wa ndoa yenu au hata viongozi wa dini na mfikie muafaka wa tofauti zenu.

Mheshimu mwenza wako na usimchukulie poa. Lolote unaloona linasababisha ugomvi kati yenu jaribu kuliweka mbali kama unataka kusonga mbele katika huo uhusiano wenu.

2. Mfadhaiko wa akili (stress)
Haijalishi nini chanzo cha stress yako. Mfadhaiko wowote wa akili unaweza kupelekea mwanamke kupungukiwa hamu yake ya kutaka kushiriki tendo la ndoa kwa haraka zaidi.

Mfadhaiko wa kama mbona sipati ujauzito, maisha magumu, kusimamishwa kazi ghafla nk vyote hivi vinaweza kukupunguzia hamu ya kutaka kushiriki tendo la ndoa haraka sana.

Mfadhaiko wa akili pia unaweza kukupelekea ukajihisi kuchoka sana jambo ambalo hupelekea kukosa hamu ya tendo kirahisi zaidi.

Tafuta namna ya kuondokana na hii mifadhaiko haraka bila kuathiri afya yako ya mapenzi. Hakuna lisilo na suluhisho, jitahidi pia usikae na tatizo lako peke yako, ongea na watu utapata tu majawabu ya yanayokusibu.

3. Pombe na uvutaji sigara
Pombe na hata sigara vyote vinasemwa hupunguza hamu yako ya kutaka kushiriki tendo la ndoa kadri unavyoendelea kuvitumia kwa muda mrefu.

Wakati kiasi kidogo cha pombe kinaweza kisiwe kibaya sana lakini kinapozidi lazima kitaleta madhara katika jambo hili. Wakati upande wa sigara haijalishi ni kiasi gani unatumia ili kubaki na afya yako nzuri ya mapenzi unashauriwa uache tu sasa hivi.

Kuongea ni rahisi kuliko kutenda si ndiyo? Unahitaji kujua kwanini unapenda kuvuta na ubadili sababu hiyo na kitu kingine kizuri. Mfano kama unavuta sababu unajisikia mpweke basi jaribu kwenda kwenye viwanja vya michezo na ujumuike na watu wengine. Pamoja na hayo hakuna lisilowezekana kama ukiamua.

4. Dawa za uzazi wa mpango
Dawa za uzazi wa mpango zinasemwa huwa zinashusha usawa wa homoni mhimu kwa mwanamke ijulikanayo kama ‘testosterone’ kwenye mwili wako na mwisho wa siku hamu yako ya kushiriki tendo la ndoa lazima itashuka.

Ongea na daktari wako kama unahisi matumizi ya dawa za uzazi wa mpango yanaweza kuwa yanahusika na kushuka kwako kwa hamu ya tendo la ndoa kuona namna nyingine mbadala nzuri ya kukusaidia kupanga uzazi wako.

5. Ufanisi mdogo wa mwanaume
Kama mwanaume ataendelea kutokumridhisha mwenza wake kwa muda mrefu mfululizo hili linaweza kupelekea mwanamke husika kupungukiwa hamu yake ya kutaka kushiriki tendo la ndoa.

Hili likitokea mwanamke uwe na akili sana juu ya namna ya kumwambia hilo mwenza wako lasivyo unaweza kuharibu kila kitu bila kujua. Usimwambie mwenza wako eti huna nguvu au huwezi kazi hivi macho kwa macho.

Kuna namna ya kuwasilisha jambo hilo kwa mwenza wako kwa namna ambayo haiwezi kumumiza. Ni vizuri pia umjulishe hilo kwani kukaa kimya pia kutaleta madhara makubwa zaidi kwa uhusiano wenu lakini tumia akili unapomjulisha.

6. Historia mbaya ya mapenzi siku za nyuma
Historia mbaya kuhusu mapenzi siku za nyuma inaweza kupelekea mwanamke akapoteza hamu ya kushiriki tendo la ndoa.

Wanawake ambao wamewahi kubakwa siku za nyuma, wamewahi kutendwa vibaya na wapenzi wao au kufanyiwa vitendo vyovyote vibaya kuhusu mapenzi siku za nyuma wanaweza kupoteza hamu ya kushiriki tendo la ndoa kirahisi zaidi.

Kutibu hili unahitaji kuonana na daktari mtaalamu wa saikolojia kwa msaada zaidi na tatizo lako litaisha.

7. Kujiona siyo mrembo vya kutosha
Siku hizi wanawake wanahangaika kuongeza makalio au hata matiti yao ili tu waonekane ni warembo zaidi.

Kutokujiona wewe ni mrembo vya kutosha kunaweza kukupelekea ukaishiwa hamu ya kutaka kushiriki tendo la ndoa.

Unatakiwa tu ujikubali kama ulivyo kama vile ulivyoumbwa na Mungu. Kila mwanaume ana sababu zake za kukupenda, wanaume wengine wanavutiwa tu na jinsi ulivyo na ubongo mzuri na akili yenye utulivu na siyo sura yako wala makalio yako.

Isitoshe hizo ni sababu za muda tu, utazeeka unadhani utaendelea kubaki hivyo miaka yote? Hivyo jikubali na amini yupo mtu anakupenda hivyo jinsi ulivyo.

Hakuna jambo baya kama kujidharau mwenyewe binafsi, wewe endelea kuwa kama ulivyo yupo mtu kwa ajili yako.

8. Baadhi ya magonjwa
Magonjwa kama Kisukari, Shinikizo la juu la damu, magonjwa ya moyo, vidonda vya tumbo, maumivu wakati wa tendo la ndoa na kansa yanaweza kupelekea mwanamke akapoteza hamu ya tendo la ndoa.

Magonjwa haya pia yanaweza kupelekea kubadilikabadilika kwa homoni za kike. Hivyo ikiwa umebainika na magonjwa haya ni mhimu upate matibabu yake kwanza ili uweze kurudi katika hali yako ya kawaida.

9. Ujauzito na kunyonyesha
Homoni huwa zinabadilikabadilika wakati wa ujauzito na wakati wa kunyonyesha, Jambo hili linaweza kuathiri hitaji lako la kutaka kushiriki tendo la ndoa.

Ujauzito unaweza kukufanya ujisikie umechoka sana na kukupelekea usijisikie hamu ya kutaka kushiriki tendo la ndoa. Punguza baadhi ya kazi ukiwa mjamzito na umfikirie zaidi mwenza wako.

Ukiwa unanyonyesha pia ni vizuri ukiwa na wasaidizi kwa ajili ya baadhi ya kazi zako ili kukupunguzia uchovu.

10. Uzee
Wakati mwanamke anafikia ukomo wa hedhi kwenye miaka 40 hivi homoni ijulikanayo kama ‘estrogen’ hushuka chini kwa kiasi kikubwa sana.

Kushuka kwa homoni hii pamoja na mambo mengine pia husababisha uke kuwa mkavu muda mwingi jambo linaloweza kupelekea maumivu wakati wa tendo la ndoa na hivyo kushuka kwa hamu moja kwa moja.

Unaweza kuwa unapakaa mafuta ya asili ya nazi au jeli ya aloe vera freshi ili kupunguza madhara haya yaletwayo na umri.

Wapo wanawake ambao kwa asili wao huwa na kiasi kidogo cha hamu cha kutaka kushiriki tendo la ndoa, lakini inapokutokea hamu hiyo inashuka ghafla na kwa kiasi kikubwa ni mhimu kutafuta ushauri wa kitaalamu ili kukabiliana na hali hiyo.



Vyakula vinavyotibu tatizo la mwanamke kukosa hamu ya kushiriki tendo la ndoa

1. Parachichi

Parachichi hujulikana pia kama mkuyati wa asili. Parachichi ni dawa ya asili ya kuamsha hamu ya tendo la ndoa. Hapa Tanzania maparachichi yanapatikana kwa wingi sana mkoa wa Kilimanjaro na hata Mbeya pia.

Parachichi lina potasiamu, vitamini B6, folic acid nk, vitu hivi vitatu ni mhimu sana katika kuongeza hamu ya kutaka kushiriki tendo la ndoa kwa mwanamke.

Potasiamu husaidia kuongeza ufanisi wa kazi wa tezi ya ‘thyroid’ ambayo yenyewe husaidia kuongeza hamu ya kutaka kushiriki tendo la ndoa kwa mwanamke kama itakuwa ipo kwenye usawa wake mzuri.

Vitamini B6 huhamasisha uzalishwaji wa homoni za kiume na ‘folic acid’ ni mhimu katika kuwezesha umeng’enywaji na kuweka sawa usawa wa protini mwilini.

Kula parachichi moja kila siku. Unaweza pia kunywa juisi ya parachichi kikombe kimoja kila siku ukiongeza asali vijiko vikubwa viwili ndani yake.

2. Ndizi



Ndizi ni tunda zuri na tamu sana, lina potasiamu na vitamini B kwa wingi viinilishe ambavyo ni mhimu ili kuamsha hamu ya tendo la ndoa na uzalishwaji wa homoni ya ‘testosterone’ kwa ujumla.

Ndizi huongeza nguvu ya mwili kwa ujumla ikiwemo nguvu za kushiriki tendo la ndoa kwa wanaume pia kwa wanawake.

Kwenye chakula chako kila siku hakikisha haikosekani ndizi ili kujitibu tatizo hili la kukosa hamu ya tendo la ndoa.

3. Mayai



Mayai yana vitamini B6 na B5 vitamini ambazo ni mhimu katika kupunguza mfadhaiko (stress) mwilini.

Mayai hayaongezi tu hamu ya kutaka kushiriki tendo la ndoa bali pia husaidia kuweka sawa homoni mwilini mambo mawili mhimu sana katika kukufanya uwe na afya nzuri ya mapenzi.

Kula mayai mawili mpaka matano kila siku. Kumbuka mayai ya kuku wa kienyeji ndiyo yanafaa kwa ajili hii na siyo ya kisasa.

Kama ni ya kukaanga basi yasiive sana kwani viinilishe vyake vinaweza kupotea kama utakausha sana kwenye moto wakati unapika.

4. Asali yenye mdalasini



Jaribu na uone tofauti! Changanya vijiko vikubwa vitatu vya asali yenye mdalasini ndani ya glasi moja ya maji ya uvuguvugu na uache mchanganyiko huo kwa dakika 15 hivi.

Kunywa nusu glasi asubuhi kabla ya chakula cha asubuhi na nusu nyingine kabla ya kwenda kulala kwa siku kadhaa hata wiki kadhaa.

Kwenye lita 1 ya asali ongeza vijiko vikubwa vitano vya mdalasini ya unga na ukoroge vizuri kabla ya kuutumia. Uhifadhi mchanganyiko huu kwenye bakuli kubwa ili iwe rahisi kuukoroga tena vizuri kila unapotaka kuutumia.

5. Vyakula vyenye vitamini C

Vitamini C huongeza hamu ya kushiriki tendo la ndoa

Vitamini C husaidia kuweka sawa mzunguko na msukumo wa damu kwenye ogani mbalimbali mwilini, hivyo hakikisha unapata vyakula hivi kila mara.

Unga wa majani ya mlonge una vitamini C kwa wingi kuliko kitu kingine chochote chini ya jua. Vingine vyenye vitamini C kwa wingi ni pamoja na juisi ya machungwa, juisi ya limau, mapera nk

Vitamini C husaidia kuongeza hamu ya tendo la ndoa kwa mwanamke.

6. Vyakula vyenye madini ya chuma kwa wingi

Kwa upande wa wanawake kwa mfano kiasi kidogo cha madini ya chuma mwilini kinaweza kupelekea tatizo la kuishiwa hamu ya tendo la ndoa, kukosa msisimko, kukosa maji maji  ukeni na hata kutokufika kileleni kirahisi.

Spinachi ina madini chuma kwa wingi, pia mbegu za maboga, dagaa, unga wa majani ya mlonge nk. Tafuta vyakula vingine vyenye madini haya na utumie mara kwa mara.

7. Viazi Vitamu


Viazi vitamu vina vitamini A na potasiamu kwa wingi. Potasiamu husaidia kuweka sawa shinikizo la damu kwa jinsia zote mbili.

Kula viazi vitamu mara moja moja ili kukabiliana na tatizo hili.

8. Tikiti maji


Tikiti maji linasemwa kuwa ni mkuyati wa asili pia kama lilivyo parachichi. Kwenye tikiti maji kuna vitu hivi vitatu mhimu sana kwa afya ya mapenzi navyo ni ‘lycopene’, ‘beta-carotene’ na ‘citrulline’ ambavyo husaidiwa kuweka mishipa ya damu katika hali ya utulivu.

Tikiti maji ni viagra ya asili inayoweza kutumika kuongeza hamu ya tendo la ndoa kwa watu wa jinsia zote mbili bila kukuacha na madhara yoyote mabaya.

Kula tikiti maji kila siku na unapokula tafuna na mbegu zake kwa matokeo mazuri zaidi.

9. Kungumanga na karafuu

Kungumanaga huongeza hamu ya tendo la ndoa

Viungo hivi viwili huondoa sumu mwilini kirahisi zaidi jambo ambalo ni zuri kwa afya yako kwa ujumla ikiwemo kuongeza hamu ya kushiriki tendo la ndoa.

Katika utafiti uliochapishwa na jarida la ‘BMC Complementary and Alternative Medicine’ imebainika wazi kwamba viungo hivi viwili kungumanga na karafuu husaidia kuongeza hamu ya tendo la ndoa huku vikiondoa tatizo la harufu mbaya mdomoni.

Vyote viwili vinaweza kutafunwa moja kwa moja kiasi kidogo kila siku au kuongezwa ndani ya vyakula na chai.

Karafuu huongeza hamu ya kushiriki tendo la ndoa

10. Lozi (Almonds)

Kuongeza hamu ya kushiriki tendo la ndoa

Lozi zina madini ya zinki kwa wingi, Vitamini E, selenium na mafuta yenye afya vitu ambavyo ni mhimu sana katika kuamsha hamu ya kutaka kushiriki tendo la ndoa na kuimarisha afya ya uzazi kwa ujumla.

Kula lozi kila siku kujitibu na tatizo hili.

11. Maji ya kunywa



Maji ni uhai. Bila kunywa maji ya kutosha kila siku ni sawa na kwenda dukani bila hela mfukoni. Maji yanahusika na kila kazi ndani ya mwili wako kuanzia kuweka sawa homoni zako, kuondoa uchovu sugu, maumivu ya kichwa, kuondoa tatizo la kuwa na uke mkavu nk

Kila siku kunywa maji ya kutosha lita 2 mpaka 3.

12. Mazoezi ya viungo



Kama unasumbuliwa na hili tatizo mazoezi ni mhimu sana kwako kila siku. Hii ni kwa sababu mazoezi husaidia kuweka sawa homoni zako na kukuondolea mfadhaiko kirahisi zaidi.

Tatizo wanawake wengi hamfanyi mazoezi labda mpaka uambiwe na daktari, mazoezi ni mhimu kwako kama ilivyo chakula.

Kama uzito wako upo juu nayo inaweza kuleta shida kwani uzito ukiwa juu homoni nazo huwa hazipo sawa. Fanya mazoezi ya kukimbia kidogo kidogo (jogging) kila siku kama una uzito uliozidi.

13. Badili mikao na staili

Kama kila siku unatumia mkao au staili ya aina moja tu inaweza kukupelekea ukaanza kukosa hamu ya kushiriki tendo la ndoa. Mapenzi ni ubunifu na ubunifu unahitajika kwa pande zote mbili.

Tatizo wanawake wengi aibu nyingi na uwoga wa kuonekana ni wahuni kwa wenza wao lakini katika hali ya kawaida hakuna ubaya wowote ukimwambia bebi wako leo tufanye staili hii na hii.

Pia badili maeneo mnaposhiriki tendo la ndoa, siyo lazima iwe kitandani kila siku. Siku nyingine fanyeni jikoni, sebuleni, bafuni, nyuma ya nyumba yenu kama kuna uwanja na uzio na hakuna mtu anaweza kuwaona pia kwenye gari lenu nk.

Siku nyingine nendeni hotelini au kwenye nyumba yoyote nzuri ya kulala wageni. Pangeni safari hata nje kidogo tu ya mji mkalale huko na mfurahie maisha yenu japo mara 1 kwa mwezi.

Pia mjulishe mmeo kwamba ni mhimu awe anakuandaa vya kutosha kabla ya kushiriki tendo la ndoa na siyo mkifika tu tayari kijeshijeshi tu, hapana hiyo haifai hasa kwa mwanamke ambaye anakosa hamu ya kushiriki tendo la ndoa.

Na hapa tena niweke msisitizo, ni wote wawili mnatakiwa kuandaana na siyo mmoja tu ndiyo amuandae mwenzake.

14. Ongeza mawasiliano



Ongea na wasiliana na mwenza wako mara kwa mara. Mawasiliano kati yako na mwenza wako ni silaha mhimu sana katika kuimarisha afya ya mapenzi baina yako na mwenza wako.

Mtumie hata sms yoyote ya utani japo mara 1 kwa siku. Kuwa wazi kumweleza lolote unalolipenda na usilolipenda katika mahusiano yenu.

Vitu vya kuviepuka

Kama una tatizo hili la kukosa hamu ya kushiriki tendo la ndoa ili kupata uponyaji kwa haraka epuka vitu hivi vifuatavyo:

Vyakula vinavyopikwa katikati ya mafuta mengi
Vyakula vya kwenye maboksi (vya dukani)
Vyakula vyenye sodiamu kwa wingi
Sukari
Chai ya rangi na kahawa
Kaffeina
Pombe
Sigara
Madawa ya kulevya
Popcorn
Kama una swali au lingine la kuongeza naomba uandike hapo chini kwenye comment. Ikikusaidia usisahau kuninunulia japo vocha.

Tafadhari SHARE post hii kwa ajili ya wengine uwapendao.

No comments:

Post a Comment